Warts Ni Nini?

Warts ni vinyama vidogo vya ngozi vinavyosababishwa na maambukizi ya virusi vya Human Papilloma Virus (HPV).

hpv

Warts hutokea wakati virusi hivi vinaingia kwenye ngozi kupitia michubuko au mikato midogo, na kusababisha ukuaji usio wa kawaida wa seli za ngozi. Ingawa warts si hatari sana, zinaweza kusababisha usumbufu na mara nyingi huwa zinahusisha aibu kwa watu.

Aina Za Warts:

Warts zinaweza kuonekana sehemu mbalimbali za mwili, na aina zake zinaweza kutofautiana kulingana na eneo la mwili zilipo na aina ya HPV inayosababisha. Zifuatazo ni baadhi ya aina za warts ambazo ni pamoja na;

1) Common Warts.

Hizi ni warts za kawaida zinazojitokeza mara nyingi kwenye mikono na vidole. Zina umbo la duara  na huweza kuwa na madoa meusi.

2) Plantar Warts.

Hutokea kwenye nyayo za miguu na zinaweza kusababisha maumivu wakati wa kutembea kutokana na shinikizo kwenye miguu.

plantar warts/

3) Flat Warts.

Hizi ni ndogo, bapa, na laini. Mara nyingi hutokea kwenye uso, mikono, au mapaja, na zinaonekana zaidi kwa watoto na vijana.

flat warts

4) Genital Warts.

Hizi hutokea kwenye maeneo ya siri, na zinaweza kuathiri uke, uume, au eneo la mkundu. Zinasababishwa na aina fulani za HPV na huambukizwa kupitia ngono.

Soma pia hii makala: Ujue Ugonjwa Wa Genital Warts (Kuota Vinyama Sehemu Za Siri) Na Tiba Yake.

5) Filiform Warts.

Hizi ni warts nyembamba na refu zinazojitokeza kwenye uso, shingo, au maeneo karibu na midomo au macho.

Mambo Yanayoongeza Hatari Ya Kupata Warts:

Kuna mambo kadhaa yanayomuweka mtu katika hatari ya kupata warts ikiwemo;

1) Kuchangia Vitu Binafsi Na Mwathirika Wa Warts.

Kuchangia (kushea) vitu binafsi kama vile taulo, nguo, viatu, na vifaa vya usafi wa mwili vinavyotumiwa na mtu mwenye warts vinaweza kuhamasisha kuenea kwa HPV.

2) Kufanya Ngono Isiyo Salama Na Mwathirika Wa Hpv.

Ikiwa unashiriki ngono isiyo salama na mtu aliyeathirika na virusi wa Hpv basi unajiweka katika hatari kubwa ya kupata warts hasa genital warts. Pia kufanya ngono kwa kutumia mdomo inakuweka katika hatari ya kupata warts au kuota vinyama sehemu za mdomo (filiform warts).

3) Ngono katika Umri Mdogo.

Watu wanaoanza ngono mapema wapo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata warts hasa genital warts kutokana na kinga za mwili kuwa chini sana.

4) Ujauzito.

Wakati wa ujauzito, mabadiliko ya homoni, mabadiliko katika mfumo wa kinga ya mwili yanaweza kuongeza uwezekano wa kupata warts hasa genital warts.

5) Kutembea Peku Katika Maeneo Ya Umma.

Kutembea bila viatu katika maeneo kama vile maeneo ya kuogelea, bafu za umma (public showers), au viwanja vya michezo kunaweza kuongeza hatari ya kupata maambukizi ya HPV na kupata warts za miguu (plantar warts).

6) Kujikuna Au Kukwaruza Ngozi.

Kukwaruza ngozi kunaweza kuvunja ulinzi wa ngozi na kuruhusu virusi vya HPV kuingia na kusababisha warts kwenye ngozi.

7) Kuwa Na Wapenzi Wengi.

Ikiwa una wapenzi wengi (multiple sexual partners) na hautumii kinga (condom) wakati wa kushiriki ngono basi unajiweka katika hatari ya kupata warts hasa genital warts.

8) Matumizi Makubwa Ya Sigara Na Pombe.

Tafiti zinaonesha kwamba watu wenye matumzi makubwa ya pombe na sigara wanajiweka katika hatari ya kupata warts hasa genital warts.

Kwa hiyo, ingawa uvutaji wa sigara na unywaji pombe si sababu za moja kwa moja za genital warts, tabia hizi zinaweza kudhoofisha kinga ya mwili na kuongeza hatari ya kuambukizwa HPV.

9) Kuwa Na Kinga Ya Mwili Dhaifu.

Watu wenye kinga dhaifu ya mwili kutokana na magonjwa kama vile VVU, kisukari, au wale wanaotumia dawa za kudhoofisha kinga ya mwili (immunosuppressants) wako kwenye hatari kubwa ya kuambukizwa HPV na kupata warts.

Dawa hizo zinaweza kutumika katika matibabu ya hali mbalimbali za afya, ikiwemo:

A) Autoimmune diseases.

Dawa hizo husaidia kudhibiti magonjwa ambapo mfumo wa kinga unashambulia tishu za mwili, kama vile:

  • Rheumatoid Arthritis
  • Lupus (Systemic Lupus Erythematosus)
  • Multiple Sclerosis

B) Baada ya Upandikizaji.

Watu wanaopatiwa viungo (organ transplant) wanapewa dawa za kudhoofisha kinga ili kuzuia mwili kushambulia viungo vilivyopandikizwa.

C) Magonjwa ya Saratani.

Katika baadhi ya matibabu ya saratani, dawa za kudhoofisha kinga zinaweza kutumika ili kuzuia mfumo wa kinga kushambulia seli za saratani au kuboresha ufanisi wa matibabu mengine.

Dawa Ya Warts:

Mbali na matibabu ya aina za warts hasa genital warts kufanyika hospitali kwa kuondoa vioteo juu ya ngozi iliyoathirika, matibabu mengine uhusisha matumizi ya dawa utakazoandikiwa na daktari na kuelekezwa namna ya kuzitumia mwenyewe nyumbani kwa siku kadhaa mpaka majuma kadhaa. 

Dawa zinazotumika ni pamoja na Podophyllin na podofilox, Trichloroacetic acid (TCA) au Imiquimod.

podophyllin

Soma pia hizi makala:

Madhara Ya Warts:

Yafuatayo ni madhara yanayoweza kutokea kwa mwathirika mwenye warts ambayo ni pamoja na;

1) Maumivu Na Usumbufu.

Plantar warts (warts zinazoota kwenye nyayo) zinaweza kuwa na maumivu makali, hasa wakati wa kutembea au kusimama, kwa sababu zinakua ndani ya ngozi kutokana na shinikizo la mwili.

Warts zinazoonekana kwenye vidole au maeneo ya mikono zinaweza kusababisha maumivu au usumbufu, hasa wakati wa kutumia mikono kwa shughuli za kila siku.

2) Kuathiri Muonekano.

Warts zinaweza kuathiri muonekano wa ngozi, hasa ikiwa zipo kwenye uso, shingo, au mikono. Hii inaweza kuathiri kujiamini na kuleta matatizo ya kisaikolojia kama vile msongo wa mawazo.

Warts nyingi, kama vile flat warts au filiform warts, zinaweza kusababisha usumbufu mkubwa wa kimaumbile.

3) Kujirudia Rudia.

Warts zinaweza kujirudia hata baada ya matibabu, kwani virusi vya HPV vinaweza kubaki kwenye ngozi. Hii inaweza kuwa tatizo kwa watu ambao warts zilienea kwa wingi au kwa wale walioathirika kwa muda mrefu.

4) Kuenea Kwa Warts Sehemu Nyingine Za Mwili.

Warts zinaweza kuenea kutoka sehemu moja ya mwili hadi sehemu nyingine, hasa ikiwa zitakwaruzwa au kuguswa mara kwa mara. Kwa mfano, warts kwenye mikono zinaweza kuenea hadi kwenye uso au maeneo mengine ya mwili.

5) Kuambukiza Watu Wengine.

Warts ni maambukizi yanayoambukizwa kwa urahisi kwa kugusana moja kwa moja na mtu aliye na warts au kugusa vitu alivyotumia kama vile taulo, viatu, au vifaa binafsi. Warts za sehemu za siri (genital warts) zinaweza kuenezwa kupitia ngono isiyo salama.

6) Hatari Ya Saratani (Genital Warts).

Ingawa warts nyingi hazisababishi saratani, baadhi ya aina za HPV zinazohusishwa na genital warts zinaweza kupelekea hatari ya saratani ya shingo ya kizazi (cervical cancer) kwa wanawake, pamoja na saratani za sehemu nyingine za siri kwa wanaume na wanawake, kama vile saratani ya uume au puru.

7) Kudhoofisha Kinga Ya Mwili.

Watu wenye kinga dhaifu, kama wale walio na VVU/UKIMWI au wanaotumia dawa za kudhibiti kinga ya mwili, wako katika hatari kubwa ya kupata warts nyingi ambazo zinakuwa sugu na ngumu kutibu.

8) Matatizo Ya Kiakili Na Kihisia.

Warts, hasa zile zinazoonekana kwenye uso au maeneo ya wazi ya mwili, zinaweza kuleta aibu, msongo wa mawazo, na kuathiri hali ya kujiamini. Pia, genital warts zinaweza kuathiri uhusiano wa kimapenzi na kusababisha mfadhaiko wa kihisia.

9) Madhara Ya Matibabu.

Matibabu ya warts kama vile cryotherapy, upasuaji, au dawa za kemikali zinaweza kusababisha maumivu, makovu, au athari za muda mfupi kwenye ngozi.

cryotherapy

Jinsi Ya Kujikinga Na Warts:

Ili kujikinga na warts unashauriwa kufanya mambo yafuatayo:

1) Kudumisha Usafi Wa Mwili.

Oga mara kwa mara na tumia sabuni safi kuosha maeneo yote ya mwili, haswa kwenye vidole, mikono, na nyayo. Safisha mikono vizuri baada ya kugusa maeneo yenye warts au sehemu za mwili zenye majeraha.

2) Epuka Kugusa Warts Za Wengine.

Usiguse moja kwa moja warts za watu wengine, kwani virusi vinaweza kuhamia kwenye ngozi yako.

Vitu kama taulo, viatu, na vifaa vya usafi vya watu wengine wenye warts pia vinaweza kusababisha maambukizi.

3) Tumia Vifaa Binafsi.

Tumia taulo, viatu, na nguo zako binafsi, hasa katika maeneo ya umma kama bwawa la kuogelea au gym.

Usishiriki (kuchangia) vitu binafsi kama vile vifaa vya kuogea au nguo na watu wengine.

4) Vaa Viatu Katika Maeneo Ya Umma.

Katika maeneo ya umma kama vile mabwawa ya kuogelea, bafu za umma, au vyumba vya mazoezi, vaa viatu vya kuogelea ili kuzuia kugusana na sakafu yenye maambukizi ya virusi vya HPV.

5) Epuka Kuchokoza Warts.

Usijaribu kukwaruza au kukata warts zako mwenyewe kwani unaweza kusababisha kuenea kwa maambukizi kwenye sehemu nyingine za mwili wako au kupeleka virusi kwa wengine.

6) Tumia Kinga Wakati Wa Ngono.

Ili kujikinga na genital warts, tumia mipira ya kondomu wakati wa ngono. Hii inaweza kupunguza hatari ya kuambukizwa HPV, ingawa si kinga kamili kwani virusi vinaweza kuambukizwa hata katika maeneo yasiyozungukwa na kondomu.

Kuwa mwaminifu kwa mpenzi mmoja na kuepuka kuwa na wapenzi wengi wa ngono pia hupunguza hatari.

7) Pata Chanjo Ya Hpv.

Chanjo ya HPV (kama Gardasil au Cervarix) inaweza kusaidia kuzuia aina fulani za HPV zinazohusishwa na genital warts na saratani ya shingo ya kizazi. Chanjo hii inashauriwa kwa vijana wa kike na kiume kuanzia umri wa miaka 9-26.

8) Kujenga Kinga Ya Mwili.

Lishe bora, kufanya mazoezi, na kuepuka uvutaji sigara kunaweza kusaidia kuboresha mfumo wa kinga ya mwili, hivyo kusaidia mwili kupambana na maambukizi ya HPV.

HITIMISHO:

Ingawa warts nyingi si hatari kiafya (benign growths), genital warts na aina nyingine za warts zinazojirudia zinahitaji uchunguzi wa daktari kwa sababu zinaweza kuhusishwa na hatari kubwa za kiafya, kama vile saratani.